We Believe JesusFé, Esperança e Nova Vida

2 Nyakati 1

Biblica® Toleo Wazi la Neno: Biblia Takatifu™ · suaíli

2 Nyakati 2 Nyakati 2 →

1Solomoni mwana wa Daudi alijiimarisha kwenye milango yote! Katika ufalme wake, kwa kuwa Bwana Mungu wake alikuwa pamoja naye, naye akamfanya mkuu mno.

2Ndipo Solomoni akasema na Israeli wote, majemadari wa maelfu na majemadari wa mamia, waamuzi na viongozi wote katika Israeli, pamoja na wakuu wa jamaa.

3Naye Solomoni na kusanyiko lote wakakwea mpaka mahali pa juu pa kuabudia huko Gibeoni, kwa kuwa huko ndiko Hema la Kukutania la Mungu lilipokuwa, ambalo Mose mtumishi wa Bwana alikuwa amelitengeneza huko jangwani.

4Basi Daudi alikuwa amelipandisha Sanduku la Mungu kutoka Kiriath-Yearimu mpaka mahali alipokuwa amepatengeneza kwa ajili yake, kwa sababu alikuwa amesimamisha hema kwa ajili ya hilo Sanduku huko Yerusalemu.

5Lakini yale madhabahu ya shaba ambayo Bezaleli mwana wa Uri, mwana wa Huri, alikuwa ametengeneza yalikuwa huko Gibeoni mbele ya Maskani ya Bwana Mungu, hivyo Solomoni na kusanyiko lote walimtafuta Mungu huko.

6Solomoni akapanda huko yalikokuwa madhabahu ya shaba mbele za Bwana katika Hema la Kukutania, na kutoa dhabihu 1,000 za sadaka za kuteketezwa juu yake.

7Usiku ule Mungu akamtokea Solomoni na kumwambia, “Omba lolote utakalo nikupe.”

8Solomoni akamjibu Mungu, “Umemwonyesha baba yangu Daudi fadhili nyingi, nawe umeniweka niwe mfalme mahali pake.

9Sasa, Bwana Mungu, ahadi yako kwa baba yangu Daudi na ithibitike, kwa kuwa umenifanya mimi mfalme juu ya watu ambao ni wengi kama mavumbi ya nchi.

10Nakuomba unipe mimi hekima na maarifa, ili niweze kuongoza watu hawa, kwa kuwa ni nani awezaye kutawala hawa watu wako walio wengi hivi?”

11Mungu akamwambia Solomoni, “Kwa kuwa jambo hili ndilo shauku ya moyo wako na hukuomba mali, utajiri au heshima, wala kifo kwa ajili ya adui zako, nawe kwa kuwa hukuomba maisha marefu, bali umeomba hekima na maarifa ili kuongoza watu wangu ambao nimekufanya uwe mfalme juu yao,

12kwa hiyo utapewa hekima na maarifa. Tena nitakupa pia mali, utajiri na heshima, ambavyo hakuna mfalme yeyote aliyekuwepo kabla yako amewahi kuwa navyo, na hakuna yeyote baada yako atakayekuwa navyo.”

13Ndipo Solomoni akaenda mpaka Yerusalemu kutoka mahali pa juu pa kuabudia huko Gibeoni, kutoka mbele ya Hema la Kukutania. Naye akatawala Israeli.

14Solomoni akakusanya magari ya vita na farasi. Alikuwa na magari 1,400 na farasi 12,000, ambayo aliyaweka katika miji ya magari na mengine akawa nayo huko Yerusalemu.

15Mfalme akafanya fedha na dhahabu kuwa vitu vya kawaida kama mawe huko Yerusalemu, mierezi akaifanya kuwa mingi kama mikuyu vilimani.

16Farasi wa Solomoni waliletwa kutoka Misri na kutoka Kue.1:16 Yaani Kilikia. Wafanyabiashara wa mfalme waliwanunua kutoka Kue.

17Waliagiza magari kutoka Misri kwa bei ya shekeli 6001:17 Shekeli 600 za fedha ni sawa na kilo 7. za fedha, na farasi kwa shekeli 150.1:17 Shekeli 150 ni sawa na kilo 1.7. Pia waliwauza nje kwa wafalme wote wa Wahiti na wa Waaramu.

2 Nyakati 2 Nyakati 2 →